MNYONGE
ATAWAHI KUPATA HAKI?
Kwa muda mrefu sasa, kumekuwa
na kilio kisichoonekana kupungua huku wananchi
wakikumbana na dhiki kuu wakiumia kutokana na janga la mahangaiko na taabu chungu nzima, chanzo chake kikiwa ni hawa
mabepari walio miongoni mwetu. Huku wakenya-wananchi wa kawaida wakiendelea kupitia shida kila uchao, wengine
wao wakilazimika kujitia kitanzi kutokana na hali ngumu ya maisha, wengine
wanaamua kuingia katika vikundi vya magaidi ambavyo vinawaahidi vikapu vinono
vinono punde baanda ya kutekeleza ‘kazi’, mabwanyenye wenye mali kama njugu
wanaendelea kutajirika hata zaidi. Si ajabu wala kusikitisha kusema kuwa
mabwanyenye wawa hawa ni ndugu na jamaa zetu, marafiki na wendani wetu
kindakindaki. Ni watu tuliowaaminia sana katika baadhi ya mambo yetu ya
kimaisha.
Watu wengi wanaoishi
katika mitaa ya mabanda wanakumbana na changamoto tofautitofauti, nyingi yazo zikiwa ni pamoja
na ukosefu wa chakula cha kutosha, uhaba wa maji safi ya kunywa na ya matumizi
ya kijumla ya pale nyumbani, magonjwa(kama vile saratani, kipindupindu na
malaria), ukosefu wa makaazi ya kutosha, mazingira machafu, hali inayotishia
sana afya ya wapendwa hawa. Yahuzunisha sana kuwaona mavijulanga wakifilia
mahospitalini, wengine wakikauka na kuzimia mikononi mwa mama zao pale nyumbani
kwa ukosefu wa matibabu na dawa. Katika habari za hivi majuzi, wengi wa
wananchi hawa wa kawaida wamelazimika sasa kuelekeza matumaini yao kwa wale madaktari
gushi ambao hawakuhitimu kuitwa madaktari na hivyo kuwapa wagonjwa madawa ambayo
pia ni gushi ambayo hulenga kuyaangamiza maisha ya watu hawa wasokuwa na hatia.
Watu wengi sasa wamejiingiza katika
biashara za kuuza madawa na wamefungua vioski vingi ambavyo wanaviita kliniki.
Wanatoa huduma kwa bei nafuu mno
ikilinganishwa na zile hospitali na zahanati na umma ambazo zina leseni na
idhini ya kutenda kazi. Kutokana na uhaba wa fedha ndipo hawa wananchi wenye
matumaini finyu hulazimika kwenda katika hivi vijikioski ili kutafuta msaada. Pongezi
tele kwa huduma ya afya kwa kujitokeza tisti na kukabiliana na swala hili.
Uhai wa mwanadamu ni
jambo nyeti sana ambalo lafaa kuangaliwa kwa makini zaidi kuliko kitu chochote
kile. Madaktari na mataabibu gushi wafaa kung’atuliwa kwenye huu ulingo wa
matibbu ili usalama wa afya ya watu wetu
unahakikishiwa.
Swala hili la vijana
kuanza kujihusisha na kujiingiza katika mambo ya kigaidi, huku wakiyahatarisha
maisha wa wananchi wa dhamani limekuwa ni kero miongoni mwa wengi wa mamilioni
ya wakenya. Kwanza, ikizingatiwa kuwa hali ya maisha kwa sasa imekuwa ngumu
kutokana na uhaba wa ajira miongoni mwa vijana, wakiwemo wale waliosoma na
kuhitimu na shahada zao katika vyuo. Ni aibu kubwa sana kukariri kuwa wapo wale
viongozi walaghai, wenye mifuko ya kaburi na wenye matumbo yasiyoshiba kama
jehanamu ambao huyanyoosha mikono yao katika ile hazina iliyotengewa vijana ili
kuwasaidia katika kuwapa ajira na kudukua pesa hizo kisha kujilimbikizia katika
akaunti zao. Na unapowapata katika mikutano na kusanyiko kule minadani,
wanajipiga vifua wakieleza vile walivyo na mioyo ya huruma ya kuwasaidia wananchi
wa kawaida na kuzipigania haki zao, wakitoa ahadi za kuwainua vijana kutoka
vuli la mauti ya ukosefu ajira. Jambo ambalo wengi wamesema miaka nenda miaka
rudi lakini hakuna tunda hata moja lililochipuka.
Ugatuzi ulipotangulizwa
katika nchi yetu hii mnamo mwaka wa 2013, wakenya walikuwa na matarajio chungu nzima,
jambo ambalo liliwasha taa ya matumaini miongoni mwa wananchi wa kawaida kwani mfumo huu ulikuja na vifurushi vya mambo
mazuri mazuri. Wananchi wangepata huduma zao moja kwa moja kutoka kwa serikali
ya jimbo(Kaunti). Huduma za afya sasa zingeboreshwa na wananchi wa kawaida wangepata
fursa ya kuyapata matibabu kwa bei nafuu, madawa ya kutosha, vifaa vya
umatibabu vya kutosha, malazi ya kutosha mle hospitalini kwa wagonjwa na akina
mama wanaoelekea kujifungua.
Kinaya cha haya yote
yalionekana pale ambapo simba walianza kuonyesha kucha zao ndefu! Kwa muktadha
wa hali halisia ya siku hizi, kuna visa vingi vya wanawake au watoto kufia
hospitalini wakati wa kufifungua, watu
wanaaga dunia wakipokea matibabu mahospitalini. Halikadhalika kumekuwa na visa si
haba vinavyosuhusu wananchi kulalamikia uhaba/ na ukosefu wa dawa za kutosha katika
hospitali na zahanati za umma, jambo ambalo limezua kero kubwa katika serikali
ya kitaifa. Si ajabu kudokeza kuwa wapo madaktari na wale wanaojihusisha na huduma
za matibabu kulaghai dawa zinazopaswa kupewa wagonjwa ili ziwape afueni, na
bila aibu wanazisafirisha kimagendo katika kliniki zao za binafsi huku
wakiwaacha wananchi wakijifilia kama nzi. Isitoshe, vyakula vya wagonjwa mle hospitalini
huchezewa karata na kuhepeshwa kijanja sana hadi nyumba za hawa wahudumu wa
afya. Wananenepa na kumetameta huku maskini hohehahe wakibaki katika hali za
ukiwa usiku na mchana. Je, huu ni ungwana? Je, huu ni utu, au uhayawani?
Ninapopita katika mitaa
kila mara hukumbana na vikundi vya watoto wa umri changa kabisa, wengi wao ni wadogo
sana kuwa katika mazingira kama yale! Mitaa yetu imesheheni machokoraa kotekote.
Wanatembea hapa na pale wakitafuta angaa ganda la muwa uliotafunwa hadi utamu
wote kuisha ili apigane na janga la njaa lililomkaba barabara. Mara mingi
utawapata wamejilaza kama magogo kwenye veranda za maduka kila asubuhi
unapopita. Wengine wana nguo zilizochanika na kuwa kama tambara la kupangusia miguu
mlangoni. Wamekonda na kukondeana, uzi kando na ni wenye afya zilizodhoofika kwelikweli.
Katika pitapita zangu
katika mtaa wa Majengo, Githurai 45, nilikutana na genge hili la vijana wa mitaani wakipunga unyunyu
katika maskani yao, ambayo huiita ‘Base’. Na baada ya mazungumzo ya ana kwa ana
na baadhi yao nilipata habari zilizonikwaruza moyo.
Baadhi yao walijipata
mitaani wakiwa machokora kutokana na sababu za kusikitisha, zingine zikiwa ni
za kukera moyo sana. Nilipigwa na bumbuwazi nilipowaona hata akina dada wakiwa
miongoni wa genge lile, wao pia wakilibingirisha gurudumu hili la maisha ya mitaani. Kunao
waliotoroka kwao nyumbani kutokana na vita na migogoro ya mashamba kati ya
wazazi wao na mababe wa mji/ kijiji. Mashamba yao yalinyakuliwa kwa mabavu na hivyo basi, mnyonge hana haki… Walikosa
wa kuwatetea na kuwasaidia kupigania haki zao. Wakajikuta mitaani. Wengine
wao akina dada walidhulumiwa kimapenzi na
vijiume vya mitaa na kutupwa kama tambara bovu huku wakiachwa na simanzi
isiyokuwa na kifani. Wengine ni kutokana tu na hali ngumu zaidi ya maisha kule
vijijini mwao ndiposa wakajikuta mitaani. Cha ajabu sana ni kukutana na wale
waliokuwa wanafunzi vyuoni na kuhitimu na shahada zao pia wakilisukuma gurudumu
lili hili la maisha hapa mtaani. Wametafuta ajira miaka nenda miaka rudi,
wameibisha milango ya ofisi karibu zote kuomba nafasi za ajira wakiwa na imani
kuwa kwa vile wamehitimu, watapata kazi zinazotosheleza shahada zao. Lakini wakashindwa
kufua dafu kwani wana majina yasiyopatikana katika kabila la mkurugenzi, ama ana
kisomo cha kiwango cha juu zaidi kuliko cha meneja. Hali hii huwaacha katika bahari
ya luja wakifikiria la kufanya na pa kuenda wasione.
Ni wazi kukariri kuwa tumeambukizwa
na hivyo kuugua kutokana na ugonjwa sugu wa ufisadi na ukabila. Bila kuzingatia
tajiriba na kiwango cha masomo ya mtu mtafutakazi, wakubwa katika afisi za umma
wanawachagua watu wa jamaa na kabila zao
ambao wengine wao hawahitimu kuingia katika kazi fulani. Uadilifu haupo tena.
Milungula inaliwa tokea vijijini hadi mijini. Kila mtu anaangalia tumbo lake na
kuwasahau wenye njaa zaidi kumliko yeye.
Kwa hivyo, ni ulimwengu
tunaosihi ndani mwake. Watu wamekosa uadilifu na kuwa kama wanyama wa porini
wasiomezeana mate. Wanyonge wameachwa bila sauti za kujitetea na kupigania haki
zao. Dunia ya leo kinachojalisha tu ni kuwa bora una pesa na mali nyingi
ndiposa utakubaliwa na jamii yenye tabaka la juu. Haijalishi una maoni mazito
kiasi gani. Asiyekuwa nacho kamwe hana la kusema ila ni kimya kimtawale. Na
wale walionavyo kila mara ni kuwanyanyasa na kuwadhulumu wasionavyo.
Ninapotia kikomo katika
makala haya, ningependa kutoa maoni yangu, kulingana na mtazamo wangu juu ya ukengeufu
tulio nao kama Waafrika ni kuwa bado hatujajielewa sisi ni akina nani.
Tumesahau kuwa kabla hatujajinyakulia uhuru mnamo mwaka wa 1963 December,
tulikuwa watumwa wa Mabepari Wakoloni na tuliwafanyia kazi kutwa kucha bila
kuchoka kwa mishahara ya kijungu jiko. Wakati mwingine hatukulipwa ila kwa makonde
na matusi. Mashamba yetu yalinyakuliwa kwa nguvu na watoto na waume wetu kupelekwa matekani. Wake zetu nao
hawakusazwa ng’o! Haki zetu tulinyimwa na hapakuwa na wa kututetea. Hali hii
ilibaadilika wakati akili zetu zilifunguka na tukawa na wazo la kupigania uhuru
wetu. Kisha tukawa na mashujaa waliojitolea mhanga kuyapoteza maisha yao kwa
kusudi la kulipa taifa uhuru. Damu ilimwagika na wengi wakaachwa bila makao. Kwa
hivyo, ni mengi yalitukia na ulikuwa
mchakato mrefu sana, lakini sitaki kwenda huko kwa sasa. Cha mno ni kuwa
wakati huo tulikuwa na umoja. Tulizungumza lugha moja, tukawa na wazo moja,
sauti moja na maono sawa. Tulipendana kama halua na satua na utamaduni huu ndio
ulitupelekea sisi kupata uhuru hatimaye.
Baaada ya nchi yetu
kupata uhuru tulifurahia matunda ya kung’ang’ana kwetu na kuahidiana mmoja kwa
mwingine kuwa hatutamwona mmoja wetu akidhulumiwa na tuketi kitako huku
tukitazama. Ilikuwa eti tupendane na kujali jirani. Yanayotendeka sasa ni
kinaya cha haya yote kwani maadili yameporomoka mioyoni mwa wanadamu Waafrika. Nilidhani
tutapendana na kubebeana mizigo mmoja kwa mwingine wakati wa msiba, kama tu
tulivyoagana…ukiwa na utu basi huwezi kumdhulumu msichana mdogo kimapenzi na
kumtupa kama kopo la msalani. Unatarajia ataishi namna gani? Hiyo mimba
uliyompachika endapo atamzaa mtoto. Je, atamtunza vipi kwanza ikizingatiwa kuwa
wewe ndiwe unawajibika? Ashakum si matusi, lakini watu kama hawa ni sharti
wachululiwe hatua kali sana za kisheria ili kukomesha kizungu hiki.
Makala na: Otieno Calleb O.
07-14-531-574
Nairobi, Kenya.
Comments
Post a Comment
Did you like the article? Leave your comment below