MAISHA YA CHUO
Kwa kawaida, kazi nzuri na bidii hupelekea matokeo kabambe na mwishowe
fanaka maishani. Hii huwa ndiyo hali kwa wanafunzi wanaofanya mtiani wao wa wa
kitaifa, KCSE ambapo wengine wao hufuzu na kujishindia nafasi katika vyuo vikuu
ili kusomea kozi ambazo zinawafaa zaidi. Huu ndio wakati utawapata wana na
binti za watu wakizikokota begi nzito nzito ardhini huku wanatembea kwa ustaha
na ujarisi wakielekea chuoni, nyuso zao zikimetameta metumetu kwa tabasamu ya
furaha. Hiki ndicho kiwango ambacho humezewa mate na wengi wa watahiniwa wa
KCSE na kila mmoja hujinyima usingizi na
starehe ili kupigania fursa hii. Wengi wanaojiunga na vyuo huwa na matarajio
mengi kuhusu maisha na mustakabali wao baada ya masomo ya chuo. Wao huwa na
mtazamo dhabiti katika masomo yao na kamwe hawataruhusu upuuzi wowote uuondoe
umakinifu wao kutoka kwa ‘kazi’ waliyokuja kuifanya mle chuoni.
Awali katika shule za upili, wengi huwa na maono makubwa makubwa ya
kuwa madaktari, wahandisi, meneja, marubani, wapasuaji wakuu, mahakimu,
wakili,wafanyibiashara wakubwa na kozi
nyingine zenye mishahara nono nono. Cha kustaajabisha mno ni kuwa utasikia wachache
sana wakitaja ualimu au hata ukose…Haya basi. Mambo hubadilika punde tu
wanapopokea matokeo yao ya KCSE. Hivyo, wao hujiunga na vyuo na kufanya zile
kozi zinazooana na ‘grades’ zao.
Wageni
chuoni
Chuo hujaa pomoni na wanafunzi kutoka pande zote za taifa. Wapo
wanaotoka vijijini, mijini na wale wenye heri walioishi jijini kama nyumbani
kwao halisi. Katika kutambua mazingira mapya na geni kabisa, wanafunzi
huzunguka kote kote chuoni kwa vikundi huku wakipiga selfie na kufurahia kuwa chuoni. Wengine huandaa sherehe, ‘Bash’ ambapo huwaalika marafiki zao
kutoka vyuo vingine, ndugu na jamaa zao ili waje wawasaidie kuidhinisha siku
ile na kuifanya yenye fanaka na kumbukumbu.
Hapa ndipo wanafunzi limbukeni hupata fursa murwa ya kujifunza mambo
mageni ya mjini, teknolojia mpya na kuanza kuona mambo ambayo hawajawahi
kuyaona maishani mwao tangu kuzaliwa. Vyumba vyenye zulia nyekundu, sakafu za mawe
ya dhamani, vyoo vya kisasa, milango yenye vijidude vya kutomaswa kisha
vinasonga vyenyewe, na mambo mengine
mengi ambayo huwaacha achama, ila kujisimamisha kadamnasi ya vyombo hivi ili
angaa wapige picha ambayo watawapelekea jamaa zao nyumbani watakaporudi likizoni.
Papa hapa ndipo wanakutana na ghorofa zenye lifti ambazo hutenda kazi kama
daladala kwa kutomasa vijidude ukutani ili kuiamurisha ikushushe katika ghorofa
ambayo ungependa. Halikadhalika, hapa ndipo wengine wao hujigundua kuwa kumbe
bado wako nyuma katika mtindo wa mavazi na hivyo basi kuanza kuiga mitindo ya
mavazi ya wale ‘wazee’ wa chuo. Maongezi pia yanabadilika katika awamu hii
maana ni wakati wa kujigundua. Wengi uhujiunga na vyama malimbali huku wakifanya
urafiki na wenzao.
Wengi hupotea njia. Hasa sana ikipatikana kuwa chuo ni kikubwa na pana. Si ajabu baadhi
ya vyuo huwapa wanafunzi wapya ramani ya chuo punde wanapoingia ili iwasaidie kupata
kumbi za mafunzo, idara mahususi na afisi ambazo wangependa kutembelea. Licha
ya hayo, kunao wengine ambao bado hupotea njia na kutokana na hili, hufika
katika kumbi za mihadhara wakiwa wamechelewa au wakose kabisa kupata ukumbi
hivyo basi kukosa kuhudhuria mhadhara. Wajuaji nao hufurahia na kujivunia
ujuaji wao.
Mijarabu na mitihani
Huu huwa ni wakati wa kubaini mbivu na bichi. Wahadhiri wa vyuo huwapa
wanafunzi takribani mijarabu miwili, moja ukiwa ni wa kufanyia utafiki na
kuwasilishwa kama kazi ya muhula, huku nyingine hupeanwa darasani na wanafunzi
huifanya kama mtihani. Mambo huwaharibikia wale ambao waliponda raha ya Campus na kukosa kuhudhuria mihadhara na
kusoma halikadhalika. Wengine hulazimika kutumia mbinu zisizo halali
kujinyakulia alama nene.
Msukumo mwingi hutokea hasa nyakati za mtihani wa mswisho wa muhula.
Utawaona wanafunzi wakifululiza(kwa msururu mrefu) maktabani asubuni na mapema,
hata Jumapili. Wengine vitabu vi mikobani, wengine wamevining’iniza viganjani na
kutembea aste aste, vichwa wamevisimamisha wima angani. Sitaki nikueleze yale hutukia
mle maktabani wakiwa wamezingirwa na furushi ya vitabu vya kila aina. Mezani pametandikwa vitabu vikubwa vikubwa huku mengine yamesimamishwa
kwenye kingo za meza, nusra vianguke. Watu wanasoma!
Nyakati za mitihani, utawapata wengine bado wangali na vijitabu kwenye
barabara za kuelekea kwenye kumbi za mitihani wakijaribu kuguguna maneno
chinichini na kuyakariri mara kadhaa kama kibwagizo cha shairi arudhi.
Baada ya mitihani ya mwinso wa muhula watu hurudi kwao nyumbani
kuungana na jamii zao baada ya miaezi mitatu.
Maisha
ya chuo
Chuoni utayastaajabia ya Musa. Ya Firauni pia utayaona vilevile kwani
ni mahali penye sura ya karakana ya jua kali. Utakutana na chochote, utakumbana
na mtu yeyote. Changamoto nazo ni chungu nzima. Lakini utafanyani? Wahenga
walisema kuwa dunia ni uwanja wa fujo. Maisha ni jani kavu, linateketezwa
motoni kisha halipo tena. Wapo wanafunzi waliotoka katika familia tajiri na
wenye mali kama mchanga baharini. Kwa upande kinyume, kuna wale waliotoka
katika aila hohehahe wanaoishi maisha ya kiganja na mdomo. Wana mapato finyu.
Walio navyo kila mara watataka kuonyesha kuwa kwa kweli wanavyo. Na
maskini pia hawatakuwa na budi kutafuta namna ya kujikimu, hivyo kuwalazimisha
kujihusisha katika shughuli mbalimbali za kutafuta namna. Wengine hulazimika
kutafuta ajira katika makampuni mjini ili angaa wapate jinsi ya kukamilisha
karo ya chuo, kulipa kodi ya nyumba na kujikimu kimaisha. Wengine hulazimika
kujiingiza katika ulingo wa biashara ambapo huuza nguo za mitumba, vyatu na matunda
katika mitaa ya chuo. Wengine hufungua vyumba vya kuonyeshea sinema. Watu
hufanya mambo mengi tu ambayo huwasaidia kujikimu maishani. Si ajabu kuwa
wengine wataingia katika biashara zisizo halali kama za kuuza dawa za kulevya
na mali nyingi nyingine gushi.
Kwa wale walio na heri, maisha kwao ni kama mswaki. Kila kitu
wanachohitaji wanacho. Kwa namna hii, wengi huwa wazembe sana hasa katika
kufanya kazi zao za muhula na hivyo kuwalipa wale wenye akili walio na mahitaji
ya pesa ili kurahisisha kazi. Ni mengi hutukia na hii yote husababishwa na
swala kuwa hakuna wa kumchunga mwanafunzi kama ilivyokuwa katika shule za upili.
Iwapo unatarajia kujiunga na chuo, ama wewe ni mzazi una mtoto ambaye
ungependa kumwingiza chuoni hivi karibuni, basi haya ni baadhi tu yay ale
hutukia mle chuoni. Zingatia ukweli kuwa wapo wanaoenda chuoni wakiwa na
matumaini mengi maishani ya kufanikiwa na hivyo basi huwa na bidii za mchwa
katika mtalaa wao lakini hapo katikati mambo hubadilika na kuwageukia. Maisha
yanawakazia kamba na wanachoweza kufanya ni kusalimu amri za kuingia katika
ulimwengu tayari kwa mapambano.
Comments
Post a Comment
Did you like the article? Leave your comment below